KISWAHILI Form 4 Topic 2

UKUAJI NA UENEAJI WA KISWAHILI ENZI YA WAINGEREZA NA BAADA YA UHURU
Mambo waliyochangia Waingereza katika Ukuaji wa Kiswahili nchini Tanzania
Elezea mambo waliyochangia waingereza katika ukuaji wa Kiswahili nchini Tanzania
Waingereza walipochukua koloni la Tanganyika kutoka kwa Wajerumani walikuta Kiswahili kimeimarika na kinatumika katika maeneo mengi ya nchi. Kwa kuwa nao walihitaji kutawala hawakupuuzia matumizi ya Kiswahili katika utawala wao japo hawakutumia Kiswahili kwa lengo la kukikuza lakini walijikuta wanakieneza na kukikuza bila ya wao kukusudia.
Waingereza walitumia Kiswahili kama nyenzo ya kusaidia shughuli zao za kiutawala. Hata hivyo kuna mambo waliyofanya waingereza yaliyosaidia kukua na kuenea kwa Kiswahili, mambo hayo ni kama yafuatayo:
Shuguli za kiuchumi
Shuguli za kiuchumi wakati wa Waingereza zilihusisha kilimo na biashara. Kwa upande wa klimo, Waingereza waliendesha kilimo cha mazao mbalimbali, na walitumia mfumo wa kuajiri vibarua kutoka sehemu mbalimbali za nchi. Vibarua hao walijulikana kwa jina la manamba.
Katika mkusanyiko wa vibarua hawa waliokuwa na usuli wa makabila tofautitofauti, lugha pekee iliyoweza kuwaunganisha ni Kiswahili ikizingatiwa kwamba Kiswahili kiliteuliwa kuwa lugha rasimi katika mawasiliano ya kiutawala. Walilazimika kuzungumza Kiswahili kwani bila hivyo mawasiliano yasingeweza kufanyika kwa urahisi.
Hata hivyo kupitia shuguli za kilimo maneno mapya ya Kiswahili yaliweza kuzaliwa, kwa mfano: yadi, belo, belingi, bani, mtama n.k, kwa hiyo kupitia shughuli hizi Kiswahili kilizidi kukua.
Shuguli za kiutamaduni
Shughuli hizi ni kama vile uigizaji wa tamthiliya za kigeni, uchezaji wa mziki wa kigeni hususani twisti. Tamthiliya za kigeni zilikuwa zikiigizwa majukwaani kwa lugha ya Kiswahili na hivyo ikasaidia kukua kwa msamiati wa Kiswahili.
Shughuli za kidini
Wakati wa utawala wa mwingereza pia kuliambatana na ujio wa wamishonari waliokuwa na lengo la kueneza dini ya kikristo.
Katika harakati hizi walitumia lugha ya Kiswahili ili kufanikisha malengo yao ikizingatiwa kwamba Kiswahili kilikuwa kimeshaenea vya kutosha wakati wa utawala wa Mjerumani, kwa hiyo wamishonari wa Kiingereza waliendelea kukiimarisha zaidi.
Pia shughuli za kidini zilipelekea kutafsiriwa kwa vitabu mbalimbali vya kidini kama vile Biblia na vitabu vingine. Tafsiri ya vitabu hivi ilikuwa ni kutoka katika lugha ya kiingereza kwenda katika lugha ya Kiswahili. kwa kufanya hivi Kiswahili kiliweza kuingiza msamiati mwingi sana na hivyo kukuza lugha ya Kiswahili.
Wamishonari walilazimika kujifunza Kiswahili hukohuko kwao ili wanapokuja huku Afrika Mashariki wasipate tabu ya kujifunza Kiswahili. Kwa sababu hii wamishonari waliokuwa wamekwishajifunza lugha ya Kiswahili walitunga kamusi za Kiswahili – Kiingereza ili kuwasaidia wenzao pia kujifunza Kiswahili; kwa njia hii waliweza kukikuza Kiswahili.
Shughuli za kisiasa
Shughuli za kisiasa hasa katika uanzishwaji wa vyombo mbalimbali vya kiutawala, jeshi, polisi, mahakama, boma n.k. Kufuatia uanzishwaji wa vyombo hivi msamiati mwingi wa Kiswahili uliweza kuzuka na hivyo kukuza Kiswahili.
Shughuli za kiutawala
Makampuni ya uchapishaji yalianzishwa (East African literature Bureau), na kamati ya lugha iliundwa (Interterritorian language committee). Hatua hii iliimarisha matumizi ya lugha ya Kiswahili hali iliyosaidia kukua kwa lugha ya Kiswahili.
Shuguli za ujenzi wa reli na barabara
Shughuli hizi pia zilisaidia kuibuka kwa msamiati mpya kama vile, reli, stesheni, tiketi n.k.
Usanifishaji wa Kiswahili
Usanifishaji wa lugha ya Kiswahili pia lilikua ni jambo jingine muhimu sana lililosaidia kukua kwa msamiati wa Kiswahili. Lengo la usanifishaji wa Kiswahili lilikuwa ni kuleta ulinganifu wa matumizi ya lugha ya Kiswahili katika ukanda wa Afrika Mashariki.
UENEAJI WA KISWAHILI
Ukuaji na Ueneaji ni maneno mawili yenye maana zinazokaribiana lakini zinazotofautiana. Ukuaji humaanisha ongezeko la msamiati katika lugha na ueneaji ni uongezekaji wa matumizi ya lugha kieneo. Kwa hiyo hapa tutaangalia yale mambo yaliyosababisha Kiswahili kitumike katika eneo kubwa. Mambo hayo ni haya yafuatayo:
Vyombo vya habari
Vyombo vya habari vilivyokuwepo kwa wakati huo ni redio, magazeti na majarida mbalimbali. Kwa upande wa redio kulikuwepo na redio Tanganyika iliyoanza kurusha matangazo yake kwa kutumia lugha ya Kiswahili. Na magazeti yaliyokuwa yakichapishwa wakati huo ni pamoja na: Mambo leo, Sauti ya Pwani, Kiongozi na Habari za leo. Magazeti haya yote yalikuwa yakichapishwa kwa lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo kwa kutumia vyombo vya habari (redio na magazeti) kiswahili kiliweza kuenea.
Kilimo
Kupitia kilimo watu waliweza kukutana pamoja, watu wa makabila tofautitofauti. Kwa hiyo katika kipindi chote walichokaa kwenye makambi ya mashambani waliweza kujifunza Kiswahili na walipomaliza muda wao walirudi nyumbani wakiwa wamejifunza lugha mpya na hivo kwa njia hii waliweza kuieneza lugha ya Kiswahili.
Muundo wa jeshi la kikoloni (KAR)
Jeshi la KAR liliundwa na watu kutoka makabila mablimbali, na lugha iliyokuwa ikitumika jeshini ni Kiswahili, askari hawa walisaidia kueneza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kwani kila walipokwenda walikuwa wakizungumza Kiswahili.
Mfumo wa elimu
Chini ya utawala wa Waingereza Kiswahili kilitumika katika masomo yote kwa ngazi ya shule ya msingi, na pia kilitumika kama somo kwa ngazi ya shule za sekondari. Kwa hiyo hii pia ilichangia kuenea kwa lugha ya Kiswahili
Harakati za kudai uhuru
Chama cha TANU kilianzisha harakati za kudai uhuru, harakati hizo ziliendeshwa kwa lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo kupitia harakati hizo Kiswahili kiliweza kuenea kwa kiwango kikubwa.
Tathimini ya maendeleo ya Kiswahili wakati wa Waingereza
Licha ya maendeleo ya lugha ya Kiswahili katika utawala wa Waingereza, pia kulikuwa na changamoto zilizoikabili lugha ya Kiswahili katika kupiga hatua ya maendeleo. Changamoto hizo ni kama zifuatazo:
Kutofundishwa kwa Kiswahili shule zote nchini
Wakati wa utawala wa Waingereza Kiswahili kilifundishwa katika shule za watoto wa kiafrika tu, wakati katika shule za watoto wa kizungu Kiswahili hakikufundishwa. Kwa hiyo suala hili lilifanya Kiswahili kipewe msukumo mdogo sana na hivyo kuhafifisha ukuaji wake.
Kutotumika kwa Kiswahili kama lugha ya kufundishia
Lugha ya Kiswahili ilitumika kufundishia katika shule za msingi pekee ilihali lugha ya kiingereza ilitumika kuanzia shule za sekondari hadi elimu ya juu. Hali hii ilisababisha watu kujitahidi sana kujifunza kiingereza; kwa kuzungumza kiingereza ilikuwa na ishara kwamba wewe ni msomi, na hivyo kutokana na hali hii Kiswahili kilendelea kukua polepole sana.
Kukosekana kwa vyombo vya kizalendo vya kukuza Kiswahili
Vyombo vilivyokuwa vinahusika na masuala ya ukuzaji wa Kiswahili wakati wa ukoloni vilikuwa vimeanzishwa na wakoloni wenyewe, kwa mfano Kamati ya Lugha ya Afrika Mashariki (Inter-Territorial Swahili Language commitee) na Shirika la maandiko la Afrika Mashariki (East African Literature Bureau). Katika hali kama hii ukuzaji wa Kiswahili ulikosa msukumo mkubwa wa kizalendo.
Kasumba ya kuthamini Kiingereza
Wananchi walikuwa na kasumba kwamba mtu anayezungumza Kiingereza alichukuliwa kuwa ni mtu mwenye maendeleo na msomi, kwa hiyo hali hii ikapelekea watu kutothamini Kiswahili na hivyo Kiswahili kudharaulika.

Shughuli mbalimbali zinazowezesha Kukua na Kuenea kwa Kiswahili nchini
Elezea shughuli mbalimbali zinazowezesha kukua na kuenea kwa Kiswahili nchini
Baada ya uhuru kuna harakati mbalimbali zilizochukuliwa na serikali ya Tanzania katika kukiendeleza na kukikuza kiswahili. Harakati hizo ni pamoja na kupendekezwa kuwa lugha rasmi 1962. Mkwaka 1964 kiswahili kilipendekezwa kuwa lugha ya taifa na kuwa kitatumika katika shughuli zote za kiserikali na kitaifa mfano katika elimu hususani elimu ya msingi.
Kuundwa kwa Chombo cha usanifishaji ambacho kilikuwa na kazi ya kuhimiza maendeleo ya kiswahili, kutayarisha kamusi na vitabu mbalimbali vya sarufi na fasihi ya lugha ya kiswahili na kuandaa wataalamu watakaoshughulikia usanifishaji wa Kiswahili
Pia baada ya uhuru kulianzishwa Taasisi mbalimbali zitakazoshughulikia lugha ya kiswahili. Mfano:- BAKITA, TUKI, TUMI, UKUTA, UWAVITA, Idara ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaamu.
Baada ya uhuru nchini Tanzania kiswahili kilienea kwa kasi kubwa sana. Kuna sababu mbalimbali ambazo zilichangia kukua na kuenea kwa kiswahili hapa nchini. Baadhi ya sababu hizo ni pamoja na kuteuliwa kwa kiswahili kuwa lugha ya Taifa, Kiswahili kitumike katika Elimu, mfano kuwa lugha ya kufundishia katika shule za msingi. Kuundwa kwa vyombo mbalimbali vya kukuza na kuneza kiswahili, Kiswahili kuwa Lugha rasmi na lugha ya Taifa, shughuli mbalimbali za kidini, shughuli za kisiasa na kiutawala na shughuli za kiutamaduni na uchapishaji wa vitabu na majarida mbalimbali.
Kiswahili kuwa lugha ya taifa
Baada ya uhuru mwaka 1962 kamati iliundwa ili kuangalia uwezekano wa kutumia kiswahili katika shughuli zote rasmi, mfano bungeni na shughuli zote za kiofisi. Pia kiswahili kiliteuliwa kuwa lugha ya taifa 1964 ambapo katika shughuli zote za kitaifa zitaendeshwa kwa kutumia lugha ya kiswahili. Hivyo kiswahili kilihimizwa kutumika katika mawasiliano yote hasa katika shughuli za umma na Wizara zote, Serikali na Bunge, kiswahili kiliendelea kupanda hadhi zaidi wakati wa Azimio la Arusha la mwaka 1967 kwani azimio hilo lilitungwa na kuandikwa kwa lugha ya kiswahili.
Kuundwa kwa vyombo vya ukuzaji na uenezaji wa Kiswahili
Tanzania baada ya uhuru ilifanya jitihada za kuunda vyombo mbalimbali vya kukuza na kueneza Kiswahili katika nyanja mbalimbali mfano wa vyombo hivyo ni UWAVITA BAKITA, TUKI, Taasisi ya Elimu,TAKILUKI na Chama cha Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam.
Kutumika katika elimu
Kiswahili licha ya kutumika katika shughuli mbalimbali za kiserikali, kilipendekezwa kutumika katika shule za Msingi na kufundishwa katika elimu ya sekondari kama somo na katika vyuo vikuu wanatoa shahada mbalimbali za lugha ya kiswahili. Pia katika Elimu ya watu wazima ambao hawakujua kusoma na kuandika. Watu hawa walijifunza masomo mbalimbali kwa lugha ya kiswahili na kuwafanya watu wengi kujua kusoma, kuandika na kuzungumza lugha ya kiswahili fasaha. Kampeni hii ilikuwa kwa nchi nzima ambapo walijifunza elimu ya Afya, Siasa, Kiswahili, Kilimo na ufundi kwa lugha ya Kiswahili na kuwafanya watu wengi kuzungumza kiswahili sanifu.
Vyombo vya habari
Tangu uhuru ulipopatikana kuna vyombo mbalimbali vya habari vilivyoanzishwa. Vyombo hivi hutumika kueneza kiswahili kwa kiasi kikubwa na hufikiwa na watu wengi licha ya kuwepo kwa changamoto za kiuchumi. Vyombo hivyo ni magazeti na majarida mbalimbali ambayo huandikwa kwa lugha ya kiswahili lakini kuna redio na runinga ambazo matangazo yake hutangazwa kwa lugha ya kiswahili. Hivyo kukifanya kiswahili kuenea kote ndani na nje ya nchi.
Biashara
Shughuli za kibiashara nchini husaidia kuenea na kukua kwa kiswahili kutokana na kuwepo kwa makabila tofauti tofauti ambapo wafanyabiashara huweza kuunganishwa kwa lugha ya kiswahili. Hivyo kiswahili hudumishwa na kutumika katika biashara hizo.
Shughuli za siasa na utawala
Tangu wakati wa harakati za kupigania uhuru kiswahili kimetumika kama nyenzo muhimu kuwaunganisha wananchi. Shughuli za kisiasa zimetumia lugha hii katika kujiimarisha; mfano wakati wa chama kimoja, Azimio la Arusha na Mfumo wa vyama vingi Kiswahili kimetumika kama njia kuu ya mawasiliano. Pia katika utawala chama kinachotawala kimekuwa na harakati za kukiendeleza kiswahilli katika nyanja zote. Ambapo kiswahili kimekuwa kikitumika katika shughuli zote za kiutawala. Hivyo shughuli za kisiasa na kiutawala zimechangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza, kukieneza na kukiendeleza kiswahili.
Uandishi na uchapishaji wa vitabu
Kuibuka kwa waandishi wa vitabu mbalimbali vya kiswahili vya sarufi na fasihi ambavyo vilichambua kwa kina mambo mabalimbali yahusuyo lugha ya kiswahili na utamaduni wake, mfano :- F Nkwera, Shabani Robart, Mathias Mnyapala na Shaffi Adam Shaffi. Waandishi wengine chipukizi walijitokeza na wanaendelea kujitokeza katika tasnia hii ya uandishi wa vitabu.
Shughuli za kiutamaduni
Shughuli za kiutamaduni zimechangia kueneza kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili. Shughuli hizo ni pamoja na harusi, misiba, matanga na sherehe mbalimbali za kijamii ambazo zimesaidia kukiendeleza Kiswahili kwa kuwa huwakutanisha watu tofautitofauti katika shughuli hizo, ambapo huwalazimu kutumia lugha ya kiswahili katika mawasiliano na kufanya kiswahili kuendelea. Pia katika Sherehe mbalimbali vikundi vya sanaa na muziki vinavyotumia lugha ya kiswahili kutumbuiza. Vikundi vingine huandaa nyimbo zao kwa ajili ya kukieneza Kiswahili.
Vyombo vya Ukuzaji na Uenezaji wa Lugha ya Kiswahili
Tangu Tanzania ipate uhuru hadi sasa kuna vyombo kadha wa kadha vilivyoanzishwa kwa ajili ya kukuza na kueneza Kiswahili baadhi ya vyombo hivyo ni hivi vifuatavyo:
BAKITA
Hii ni taasisi ya serikali iliyoundwa kwa sheria ya Bunge Na.27 ya mwaka 1967 kwa madhumuni ya kukuza Kiswahili. Kutokana na sheria hii Baraza ndilo mratibu wa kusimamia asasi zote na mawakala wote wanaokuza Kiswahili katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
BAKITA imekuwa na mchango mkubwa sana katika ukuzaji na uenezaji wa lugha ya Kiswahili kupitia majukumu yake. Majukumu ya Baraza kama yalivyofafanuliwa katika sheria hiyo ni haya yfuatayo:
  • Kuratibu na kusimamia maendeleo na matumizi ya Kiswahili nchini kote. Katika kufanya hivi Baraza lina jukumu la kuhakikisha Kiswahili kinaendelea na kuhakikisha kuwa matumizi ya Kiswahili yanakuwa sahihi.
  • Kushirikiana na vyombo vingine nchini vinavyojihusisha na maendeleo ya Kiswahili na kuratibu shughuli zao. Vyama vya Kiswahili kama vile CHAKAMA, CHAWAKAMA vina mchango mkubwa wa kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili kwa kushirikiana na BAKITA. Ushirikiano wa BAKITA na vyama hivi waweza kuwa ni wa kuto ushauri, au msaada wa kifedha, kwa mfano BAKITA imekuwa ikiwasaidia CHAWAKAMA pale wanapokuwa wanataka kufanya makongamano nap engine wanahitaji msaada wa kifedha, kwa hiyo BAKITA imekuwa ikiwasaidia kifedha.
  • Kuhimiza matumizi ya Kiswahili katika shughuli rasmi na za kawaida. BAKITA imekuwa ikiandaa vipindi mbalimbli redioni ili kuhimiza matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili.
  • Kushirikiana na mamlaka zinazohusika kuthibitisha tafsiri sanifu za istilahi. Katiaka uundaji wa istilahi, BAKITA imekuwa ikichapisha vitabu mbalimbali ikionesha istilahi sanifu zilizoingizwa katika lugha ya Kiswahili. kwa hiyo kupitia jukumu hili Kiswahili kimekuwa kinakua.
  • Kutoa huduma za tafsiri na ukalimani kwa serikali, mashirika ya serikali na yasiyo yaserikali na asasi nyingine. Kupitia tafsiri zinazofanywa na BAKITA Kiswahili kimekuwa kikikuwa na kuenea.
  • Kuchapisha jarida au toleo linalohusu lugha na fasihi ya Kiswahili. Machapisho haya ya BAKITA yanaendelea kukifanya Kiswahili kukua kwa kuongeza msamiati mpya na hivyo watu wanaposoma machapisho hayo wanajifunza msamiati mpya na hivyo kufanya Kiswahili kukua.
  • Kushirikiana na mashirika ya kitaifa, asasi na watu binafsi, kufuatilia, kushauri na kusimamia shughuli zinazolenga kukuza Kiswahili nchini Tanzania.
  • Kutoa ushauri kwa waandishi na wachapishaji ili watumie Kiswahili fasaha. Kwa kufanya hivi matumizi bora ya Kiswahili yanakuwa yanaimarika.
  • Kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuthibitisha vitabu vya Kiswahili vitakavyotumika shuleni na vyuoni kabla havijachapishwa. Hili pia ni jamabo linaloimarisha matumizi ya Kiswahili sanifu.
TAKILUKI
Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI) ilianzishwa mwaka 1979 kwa lengo la kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya Zanzibar, ili kutimiza lengo hilo TAKILUKI inajishughulisha na kazi zifuatazo:
  • Kuratibu na kuendesha mafunzo ya lugha ya Kiswahili visiwani Zanzibar, kuendesha mafunzo ya lugha ya Kiswahili kwa wazawa na wageni, kuhariri miswada mbalimbali ili kuthibitisha ufasaha wa Kiswahili na kufanya tafiti za Kiswahili katika Nyanja zake zote, hususani katika uwanja wa sarufi na fasihi.
  • Pia TAKILUKI wana kazi ya kuandaa istilahi za taaluma mbalimbali, kutoa huduma za taaluma mbalimbali, kutoa huduma za tafsiri na ukalimani kwa lugha mabalimbali kwa mashirika, idara, wizara, taasisi, kampuni na watu binafsi, kufundisha lugha za kigeni na kuandika vitabu mbalimbali vya Kiswahili.
  • Pia hujishughulisha na utoaji wa ushauri wa kitaaluma kwa watunzi wa vitabu ili waweze kuandika kazi zenye ubora, na kushirikiana na wadau wengine wa Kiswahili kama vile, mashirika, wizara, taasisi, vyuo na watu binafsi katika kuendesha shuguli za ukuzaji wa Kiswahili, mathalani kuandaa na kuendesha semina, warsha na kozi fupifupi za Kiswahili.
  • Vilevile hujishugulisha na usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili katika vyombo vya habari na katika shughuli mbalimbali za serikali na za kawaida.
TUKI/TATAKI
Majukumu ya TUKI ni pamoja na kuunda sera muafaka za kustawisha Kiswahili na pia kufanya utafiti katika lugha ya Kiswahili.
Majukumu mengine ya TUKI ni kuhariri, kuchapisha vitabu na kutawanya vitabu na majarida ya kitaaluma katika Kiswahili.
Kwa sasa TATAKI inatoa shahada ya awali na uzamili katika lugha ya Kiswahili, kwa njia hii inawaandaa wataalamu wa lugha ya Kiswahili ambao watatumika sehemu mbalimbali za ulimwengu kufundisha lugha ya Kiswahili.
CHAUKIDU
CHAUKIDU ni kifupi cha Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani, makao makuu ya chama hiki kwa sasa yapo chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani
Madhumuni makuu ya CHAUKIDU ni: Kuwajumuisha pamoja wakuzaji wa Kiswahili duniani kote kwa lengo la kuchochea kasi ya malengo mahususi yafuatayo:
  • Kukuza Kiswahili katika nyanja zote ambamo lugha hii inatumika au inaweza kutumika na kuongeza ufanisi wa mawasiliano katika ufundishaji na utafiti wa maarifa ya aina zote, uandishi/utangazaji wa habari, uandishi wa vitabu, uchapishaji vitabu na majarida, utayarishaji wa safari za mafunzo katika Afrika ya Mashariki na Kati, n.k.
  • Kusambaza habari na matokeo ya utafiti kwa kutumia machapisho mbalimbali na teknolojia ya mtandao wa kompyuta juu ya vipengele mbalimbali vya Kiswahili na masuala yanayohusiana na Kiswahili.
  • Kuwajumuisha wanachama kwa ajili ya kubadilishana mawazo na tajiriba zao katika masuala mbalimbali yanayohusu Kiswahili (k.v. uboreshaji wa ufundishaji, utangazaji, utafiti, uandishi, nk.) kwa njia ya mkutano wa kila mwaka, warsha au semina au kongamano maalumu, na hata kwa njia ya mtandao.
  • Kuelimisha umma juu ya umuhimu wa kujivunia, kuendeleza, na kuheshimu Kiswahili.
  • Kushauri ama kushinikiza serikali za nchi ambamo Kiswahili kinazungumzwa kutambua thamani iliyobebwa na maliasili hii ili kuunda sera muafaka za kukiendeleza kadri ya uwezo wake kwa manufaa ya maendeleo ya serikali na watu wake kijamii, kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, kielimu, n.k.
CHAWAKAMA
CHAWAKAMA husimama badala ya Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili vyuo vikuu Afrika Mashariki. Chama hiki kilianzishwa mwaka 2004 kwa lengo la kukuza na kueneza Kiswahili katika eneo lote la Afrika Mashariki kupitia wanafunzi wanaosoma Kiswahili vyuoni. Wanachama wa chama hiki ni wale wanosoma Kiswahili na hata wale wenye mapenzi ya lugha ya Kiswahili pia wanaweza kujiunga na chama hiki.
Chama hiki kina utaratibu wa kuandaa makongamano ambapo wanachama wake kutoka nchi zote za Afrika Mashariki hupata fursa ya kukutana mara moja kila mwaka. Pamoja na utaratibu wa chama kuandaa makongamano pia uanzishwaji wake umeambatana na malengo kadhaa ambayo ndiyo dira inayoiongoza chama kwa mujibu wa katiba, malengo hayo ni haya yafuatayo:
  1. Kuwapa wanachama nafasi ya kujadili, kuimarisha, kuendeleza na kukuza vipawa vyao vya lugha na fasihi ya Kiswahili.
  2. Kuamsha ari ya mapinduzi ya utamaduni wa lugha ya kiswahili.
  3. Kueneza lugha ya kiswahili ndani na nje ya nchi.
  4. Kushirikiana na vyama vingine katika juhudi za kuendeleza na kuimarisha lugha ya kiswahili ndani na nje ya nchi wanachama.
  5. Kuwaunganisha wanafunzi wa kiswahili Afrika Mashariki na kati katika kukikuza kiswahili.
  6. Kushirikiana na asasi mbalimbali zinazojihusisha na ukuzaji na uenezaji wa kiswahili ndani na nje ya nchi kama vile BAKITA, TATAKI, TAKILUKI, UWAVITA, CHAKAMA, BAKIZA n.k.
  7. Kuchapisha kijarida cha chama na machapisho mengine ili kusaidia kueneza taaluma ya kiswahili.
  8. Kuweka kumbukumbu ya wataalamu wa kiswahili kwa nia ya kuwatumia katika kufanikisha malengo ya chama na wadau wa Kiswahili.
  9. Kuratibu makongamano na mijadala mbalimbali inayohusiana na taaluma ya kiswahili.
Pamoja na malengo hayo, lengo kuu la chama hiki ni kueneza Kiswahili lakini sasa wanakienezaje? Wanachama wa chama hiki ambao ni nchi wanachama wa jumuia ya Afrika mashariki wanakawaida ya kuandaa makongamano kwa ngazi ya kitaifa na ngazi ya kimataifa.
Kwa ngazi ya kitaifa kila nchi huandaa kongamano kila mwaka ambalo linawakutanisha wanachama wote kutoka vyuo mbalimbali katika nchi husika. Katika kongamano hilo mada mbalimbali zinazohusu lugha ya Kiswahili na mustakabali wake hujadiliwa lakini pia maazimio mbalimbali huchukuliwa juu ya maendeleo ya chama. Sasa katika mijadala kama hii inatoa nafasi ya Kiswahili kukua kwani makala mbalimbali huandikwa ambazo pia husomwa na watu mbalimbali. Makala hizi pia zimekuwa zikichapishwa katika majarida ya chuo husika na pia zimekua zikichapishwa mtandaoni ambapo hutoa fursa kubwa kwa watu wengi zaidi kuzifikia na kusoma, hivyo kwa njia hiyo Kiswahili kinakua kimeenea.
Dhima ya kila Asasi inayokuza Kiswahili
Elezea dhima ya kila asasi inayokuza Kiswahili
Mafanikio na Changamoto Zinazovikabili Vyombo vya Ukuzaji wa Kiswahili
Mafanikio
  • Vyombo vya ukuzaji wa Kiswahili vimejitahidi sana kukuza lugha ya Kiswahili, kwa hali ya Kiswahili ilivyo sasa ni matokeo ya juhudi za vyombo hivyo. Mafanikio ya vyombo hivyo ni pamoja na haya yafuatayo:
  • Machapisho ya lugha ya Kiswahili ni mengi sana nchini na nje ya nchi, kufanya mafunzo ya Kiswahili, kukua kwa matumizi ya Kiswahili na kuongezeka kwa idadi ya watumiaji wa Kiswahili nchini.
  • Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika sehemu rasmi hasa katika ofisi za serikali na ofisi za watu binafsi inadhihirisha mafanikio ya jitihada za vyombo hivi kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili.
  • Kufundshwa kwa lugha ya Kiswahili kama taaluma kwa ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu. Hizi ni jitihada za TATAKI katika kuhakikisha kunapatikana wataalamu wa lugha ya Kiswahili, hivi sasa TATAKI wanafundisha lugha ya Kiswahili kwa ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu.
  • Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika vyombo mabalimbali vya kimataifa, matumizi ya lugha ya Kiswahili katika vikao vya Umoja wa Afrika na pia ufundishwaji wa lugha ya Kiswahili katika vyo mabalimbali Duniani ni ishara tosha ya kuonesha mafanikio ya jitihada za vyombo vya ukuzaji na uenezaji wa Kiswahili.
Changamoto
  • Vyombo hivi vinakabiliwa na upungufu wa wataalam. Wataalamu wengi waliobobea katika taaluma za Kiswahili wanakimbilia nje ya nchi wakidhani huko ndiko kuna maslahi mazuri zaidi.
  • Upungufu wa fedha za kuendeshea shughuli za ukuzaji wa Kiswahili katika vyombo hivi pia limekuwa ni tatizo sugu. Kwa hiyo shughuli za ukuzaji wa Kiswahili zinakuwa zinakwenda taratibu.
  • Taasisi hizi pia zinashindwa kujitangaza vizuri kutokana na kwamba hazina vyombo vya habari binafsi ambavyo vingeweza kutumika kutangaza shughuli zao. Jambo hili limesababisha vyombo hivi kushindwa kutoa elimu ya Kiswahili kwa kutumia vyombo vya habari kutokana na kwamba gharama za kufanya hivyo ni kubwa.
  • Vyombo hivi baadhi havina ofisi za kudumu, na hivyo kuhamahama jambo ambalo linaathiri utendaji kazi wa vyombo hivyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.

Back to top button
Close

Adblock Detected

We've noticed that you're using an adblocker. Our website relies on ads to provide free content. Please consider disabling your adblocker support us. Thank you for your support.